Magufuli ampa Mbalawa siku 7
Rais John Magufuli amesema ameanza ziara yake mkoani rukwa vibaya na kwa majonzi kutokan na ujenzi wa miradi ya maji yenye thamani ya Sh bilioni 20 kutekelezwa na mkandarasi Fally Enterprises asiye na sifa wala uwezo ambaye ameagiza achunguzwe na kushitakiwa.
Kutokana na hali hiyo amemuagiza Waziri wa maji, Profesa Makame Mbalawa kuchukuliwa hatua kali watendaji wa wizara yake waliohusika kumpatia kazi nyingi zaidi mkandarasi huyo kinyume cha taratibu.

Aidha amemuagiza Profesa Mbalawa na kumpatia siku saba kuunda tume maalumu ya uchunguzi wa kina miradi yote inayotekelezwa na mkandarasi huyo ikiwemo ile ambayo haijakamilishwa.
Mbali ya wizra ya maji pia  ameagiza Tamisemi, Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga, mkoa wa Rukwa, kamanda wa Polisi wa Mkoa, Taasisi ya kuzuia na kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoa na Wakili wa Serikali kufuatilia tuhuma dhidi ya mkandarasi huyo pamoja na hujuma uliofanywa katika Mradi wa maji Laela.
Pia amempigia simu na kumuagiza Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini, (IGP) Simon Siro kumuondoa Ofisa Mnadhimu, Polycarp Urio kwa kushindwa kutekelezwa kwa agizo la Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola akiwa ziarani Rukwa hivi karibuni.\
Rais Magufuli ametoa maagizo hayo jana katika mji mdogo  wa Laela Halimashauri ya Wilaya ya Sumbawanga kabla ya kuzindua barabara ya Tunduma-Laela-Sumbawanga kilometa 223.2 iliyogharimu Sh bilioni 375.
Mradi huo wa barabara ulikamilika kujengwa tangu mwaka 2015 kwa ufadhili wa serikali ya Marekani kupitia shirika lake la Millennium Challenge (MCC) na fedha za ndani za serikali ya Tanzania kwa kiwango cha lami.
“Huyu mkandarasi Fally hamalizi ujenzi wa miradi huku mingine ikiwa chini ya kiwango, nashangaa amepewa miradi yote.. lakini hajafutiwa usajili kwa mujibu ya sheria namba 15 ya 1994” alieleza Rais Magufuli.
“Waziri andaa wizara maalumu ichunguze miradi yote ya maji anayoijenga pia ifanyiwe upya tathimini pamoja nakubaini kama utaratibu wa manunuzi umefuatwa kwa mujibu wa sheria. Kama mkandarasi huyo amelipwa waziri baada ya kuwasilisha Certificate zote mlipaji awekwe ndani kwa mjibu wa sheria” alizidi kuagiza Rais Magufuli.
Alimwagiza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Tamisemi), Selemani Jafo kumfuatilia Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga Nyangi Msemakweli kama amemlipa mkandarasi huyo.
Mkandarasi huyo anatuhumiwa kuhujumu miradi ya maji kwa kuijenga kwa viwango hafifu ukiwemo mradi wa maji wa Laela wa gharama ya zaidi ya Sh bilioni 1.7 ukiwa umemalizika miaka mitatu iliyopita lakini maji hayatoki.
Miradi iko katika Katika Wilaya za Kalambo Nkasi na Sumbawanga.
“Ninazo taarifa kuwa Profesa Mbalawa ulipokuwa Mkoani Rukwa kikazi aliagiza mkandarasi Fally akamatwe lakini akaachiwa. Nataka nimfahamu nani aliyemuachia huru akikaidi agizo la Waziri ambaye ni mteule wangu” amehoji huku akiwataka viongozi wasitishwe na watu wenye fedha.
 Awali, Mbunge wa Nkasi Kasikazini, Ally Kessy alimweleza Rais Magufuli kuwa mkandarasi Fally hana sifa na viwango, na amefisadi miradi ya maji huku akijilimbikizia mali kwa kujenga maghorofa sehemu mbalimbali.
“Mheshimiwa Rais mafisadi kama Fally wanastahiki adhabu kali ya kunyongwa pia azitapike fedha zote kama wengine wanavyozitapika” alisema mbunge huyo machachari.
Baada ya kuzindua barabara, Rais alifika kituo cha polisi wilaya ya kipolisi ya Laela na kumpgia IGP Sirro na kumuagiza amfukuze mnadhimu Urio kwa kushindwa kumpatia RPC majina tisa ya asikari polisi ambapo waziri Lugola aliagiza wahamishwe kwa makosa ya kuwabambikizia kesi wananchi na kuwanyima dhamana.
Rais Magufuli ambaye alitokea mkoani Songwe alikokuwa kwa ziara ya kikazi ya siku tatu, jana alianza ziara mkoani Rukwa ambayo inaendelea leo. Akimaliza mkoani humo atakwenda kwa ziara nyingine mkoa wa Katavi.
MWISHOO….